IQNA

Waislamu Italia

Waislamu nchini Italia wanatarajia serikali mpya italinda uhuru wa kidini

14:41 - September 27, 2022
Habari ID: 3475847
TEHRAN (IQNA) – Mtazamo hasi dhidi ya Waislamu milioni 3 na zaidi wanaoishi nchini Italia hautarajiwi kutoka kwa serikali ijayo ya mrengo wa kulia, jumuiya za Kiislamu nchini humo zilisema.

Serikali mpya itaundwa baada ya uchaguzi mkuu wa Jumapili.

Waislamu "wanatarajia" kufanya kazi na baraza jipya la mawaziri kuhusu uhuru wa kidini unaohakikishwa na katiba ya nchi hiyo ya Ulaya.

Mabadiliko madhubuti katika uongozi wa Italia sasa yanatarajiwa. Mrengo wa kulia ukiongozwa na Giorgia Meloni, kiongozi wa chama cha Madugu wa Italia (Fratelli d'Italia), chama ambacho kijadi kinafungamana na mrengo wa kulia, kilipata wingi wa kura katika matawi yote mawili ya Bunge.

Katikati ya Oktoba, Meloni ataombwa na Rais Sergio Mattarella kuunda serikali mpya.

Kisha atakuwa waziri mkuu mwanamke wa kwanza nchini Italia, akiongoza serikali itakayokuwa ya kwanza ya mrengo mkali wa kulia tangu Vita vya Pili vya Dunia.

Uongozi mpya unatarajiwa kuwa mgumu zaidi kuliko serikali zilizopita juu ya wahamiaji haramu, lakini hakuna kinachotarajiwa kubadilika katika mtazamo mzuri wa jadi wa Italia kuelekea Mashariki ya Kati na ulimwengu wa Kiarabu.

Wachambuzi wa masuala ya kisiasa wa Italia pia wanaeleza kwamba baraza jipya la mawaziri halitarajiwa kuwa na msimamo mkali dhidi ya Waislamu nchini humo, hasa kwa vile Ligi (Lega), chama cha chuki dhidi ya wageni na wahamiaji kinachoongozwa na Matteo Salvini, kilifanya vibaya katika uchaguzi huo.  Ligi bado kitakuwa sehemu ya wengi, lakini itashikilia sauti isiyo na nguvu zaidi.

"Tuna uhakika kabisa kwamba kila serikali ya Italia itaheshimu katiba, ambayo inajumuisha katika kanuni zake za msingi uhuru wa kuabudu. Tunatarajia serikali mpya itakuwa makini na haki za jumuiya za Kiislamu,” Yassine Lafram, rais wa Muungano wa Jumuiya za Kiislamu za Italia, amesema.

Lafram ameongeza kuwa, kwa Waislamu nchini Italia, "bado kuna matatizo mengi, kuanzia makaburi ya Kiislamu hadi haja ya kuwa na sheria inayodhibiti ujenzi wa maeneo ya ibada kwa ajili ya dini zote."

Pia alielezea matarajio kwamba kutakuwa na makubaliano rasmi kati ya serikali ya Italia na jumuiya zake za Kiislamu kuandikwa hivi karibuni.

"Ni kwa manufaa ya serikali mpya kwamba kuwe na utambuzi kamili wa kisheria wa jumuiya za Kiislamu. Jambo hili litakuza utangamano,” alisema.

"Tunatarajia mengi kutoka kwa serikali ambayo inaahidi kuwakilisha Waitaliano wote. Jumuiya za Kiislamu za Italia haziwezi kushutumiwa kuwa karibu na misingi ya Kiislamu. Sisi sote ni raia wa Jamhuri ya Italia ambao wanahisi wao ni sehemu muhimu ya jamii ya Italia," Lafram aliongeza.

3480637

captcha